Sunday, August 4, 2013

KAHAMA YAANZA MIKAKATI YA KUWAOKOA MAKAHABA KWA KUWAWEZESHA KIUCHUMI



Zaidi ya wanawake tisini wanaofanya biashara ya ngono wilayani Kahama mkoani Shinyanga wanatarajia kunufaika na mradi mpya wa kuwakomboa kutoka kwenye biashara hiyo, unaoratibiwa na HUHESO Foundation kwa ufadhili wa Rapid Funding Envelop (RFE).

Hayo yameelezwa leo na Mkurugenzi wa shirika hilo Juma Mwesigwa wakati wa utambulisho wa mradi huo kwa wadau na waandishi wa habari katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa Kaltas mjini Kahama.

Mwesigwa amesema lengo la mradi huo ni kupunguza kasi ya maambukizi ya UKIMWI na kuwaondoa wanawake wanaofanya biashara ya Ngono  wilayani humo. Mwesigwa amesema kuwa wanawake arobaini watapatiwa mafunzo ya cherehani na baada ya mafunzo kila mmoja atapatiwa cherehani yake mpya huku wengine hamsini wakipatiwa mafunzo ya ujasiriamali.

Awali akizinduwa rasmi mradi huo, Kaimu mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa Kahama Lucas Makurumo aliwata wananchi kuupokea na wakina dada wajiunge pasipo woga kwa faida zao na Taifa kwa ujumla.

Mradi wa kuwakomboa wanawake wanaofanya biashara ya ngono wilayani Kahama utakaotekelezwa ndani ya mwaka mmoja unatarajia kugharimu zaidi ya shilingi milioni 146. Mradi huo utatekelezwa katika kata Malunga, Mohongolo, Kahama Mjini, Nyihogo, Nyasubi, Nyahanga, Majengo, Mwendakulima, Kagongwa na Mungula.